Na Mwandishi Wetu
MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP) imeitaka
 Serikali kuwawajibisha mara moja mawaziri, manaibu waziri na watendaji 
wakuu wa Serikali na mashirika ya umma ambao wametajwa kuhusika na 
matumizi mabaya ya fedha za umma ama kushindwa kusimamia rasilimali za 
taifa.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es 
Salaam na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Anna Kikwa (PICHANI) katika
 taarifa yake aliyoisambaza kwa vyombo vya habari. Aidha amemtaka mkuu 
wa nchi awafute kazi watendaji wanaotumia vibaya fedha za umma na 
kuwaongezea wananchi umasikini, ili iwe fundisho kwa watendaji wa 
Serikali wenye tabia kama hiyo na wachukuliwe hatua za kisheria.
Hata hivyo TGNP imeishauri Serikali 
kuboresha mifumo ya kusimamia rasilimali za nchi yetu ili wananchi wote 
waweze kufaidi keki ya taifa kwa sababu mara zote Serikali imekuwa 
ikisema Tanzania hatuna rasilimali lakini hali halisi ni kwamba 
rasilimali za taifa zinaliwa na mafisadi wachache wa ndani na nje ya 
nchi.
Katika hatua nyingine, mtandao huo umetoa 
pongezi kwa wajumbe wa Kamati za Kudumu za Bunge za Hesabu za Mashirika 
ya Umma (POAC), Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Kamati ya Hesabu za 
Serikali Kuu, Ardhi Maliasili na Utalii kwa kusimamia vema na kudhibiti 
matumizi mabaya ya fedha za serikali zinazotokana na walipa kodi na 
kuwasilisha ripoti zao Bungeni ambazo zimeibua uozo mkubwa na kujenga 
mjadala mpana unaotaka uwajibikaji kwa wanaohusika.
“Tunawapongeza pia baadhi ya wabunge 
 walioshiriki katika mijadala  kwa kuzijadili ripoti hizo kwa undani 
bila kujali urafiki, itikadi za kisiasa, hasa ile ya Mkaguzi na Mdhibiti
 Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa  kuibua  uozo uliojificha na 
kusimamia maslahi ya Taifa.” amesema Bi. Kikwa katika taarifa hiyo.
“Tumeshuhudia mara kadhaa kupitia vyombo 
vya habari  wabunge wakiacha itikadi zao za kisiasa na kusimamia kwa 
dhati dhana ya kushinikiza uwajibikaji katika vyombo vinavyohusika 
kutokana na ufisadi kama Richmond, Dowans nk. Hata hivyo, TGNP kwa muda 
mrefu tumekuwa tukipinga ubadhirifu wa fedha za umma  na kudai haki ili 
kutokomeza ufisadi uliokithiri, lakini bado ufisadi umezidi kushamiri 
hasa katika Wizara na taasisi za umma.
“Sisi kama wanaharakati tunasema kuendelea
 kwa ufisadi ni aibu kwa serikali iliyoko madarakani, TGNP tuko mstari 
wa mbele  kushinikiza rasilimali za taifa ziwanufaishe wananchi wote, 
hasa walioko pembezoni, kamwe hatutanyamazia aina yoyote ya ubadhirifu 
na matumizi mabaya ya fedha za miradi ya wananchi zilizotengwa kwa ajili
 ya maendeleo ya wananchi.” Imesema taarifa hiyo.
"Tumeshuhudia wanawake na wasichana 
wakiendelea kuwa maskini na kukumbana na mifumo kandamizi kwa kukosa 
haki za kufikia huduma za msingi kama vile maji, barabara, afya, elimu, 
kilimo, utawala bora n.k. Fedha zinazopotea zinatokana na kodi za 
wananchi na jamii ina haki ya kuhoji uwajibikaji na wahusika wanatakiwa 
kuchukuliwa  hatua za kisheria," imeongeza taarifa hiyo kwa vyombo vya 
habari.
Vilevile tunawapongeza wabunge wote 
walioshiriki kwa dhati katika zoezi la kusaini kusudio la kutaka 
viongozi waliotajwa/kutuhumiwa  kwenye ripoti hizo kuwajibika. Ili 
kuonesha dhana ya uwajibikaji na utawala bora unaozingatia misingi ya 
haki za binadamu.
No comments:
Post a Comment