NA BASHIR NKOROMO
Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika kikao chake 
kilichofanyika jana mjini Dodoma chini ya Mwenyekiti wake Rais Jakaya 
Kikwete imeibuka na masuala mazito kadhaa, ambayo leo, Katibu wa NEC, 
Itikadi na Uenezi Nape Nnauye (pichani) ameyaeleza wakati akizungumza na
 waandishi wa Habari, Katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya Chama Cha 
Mapinduzi (CCM), Lumumba jijini Dar es Salaam.
Moja ya mambo ambayo Nape amezungumzia, ni kuhusu Kamati Kuu hiyo 
kuwahoji Mawaziri saba, kujibu kero au mambo kadhaa ambayo yaliibuliwa 
wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana iliyomalizika 
hivi karibuni katika mikoa ya Mtwara, Ruvuma, Mbeya na Njombe.
Nape  alisema, Kamati Kuu iliwahoji mmoja baada ya mwingine, 
kuanzia saa tano asubuhi hadi jioni, baada ya kila mmoja kufika akiwa 
ameandaa majibu ya tuhuma au hoja alizokuwa ametakiwa kujibu mbele ya 
Kamati Kuu hiyo.
"Kwa kuwa mawaziri hao tulikuwa tumeshawapelekea hoja zinazowahusu
 ambazo tulizipisha kwa kiranja wao Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wengi 
wao walifika wakiwa na mafaili yenye majibu, ambapo waliingia na 
kujieleza mmoja baada ya mwingine, na baada ya maelezo ya kila mmoja 
wajumbe walitoa mapendekezo kwa Mwenyekiti, Rais Jakaya Kikwete", 
alisema Nape.
Hata hivyo Nape alisema, si vema kueleza kwenye vyombo vya habari 
kuhusu mapendekezo ambayo Kamati Kuu ilimshauri Mwenyekiti kuchukua, 
akisema kufanya hivyo itakuwa sawa na kumshinikiza kiongozi huyo 
kutekeleza mapendekezo yao kwa lazima na hivyo kuharibu maana nzima ya 
ushauri.
"Sisi tulichofanya ni kumpa mapendekezo, naye kwa mujibu na namna 
atakavyoona inafaa, atachukua hatua, ambavyo si lazima kumfukuza Waziri 
Kama wengi wanavyotaka iwe, bali anaweza kuchukua hatua yoyote ili mradi
 yeye mwenyewe kwa mamlaka aliyo nayo ataona ina manufaa yatakayotoa 
majibu ya kero zilizosaababisha kila mmoja wa mawaziri hao kuitwa mbele 
ya Kamati Kuu", alisema Nape.

No comments:
Post a Comment