Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Monday, July 23, 2012

JK ARUSHA DONGO MBEYA, AAHIDI KUTEKELEZA AHADI ZAKE ZOTE



RAIS Kikwete amezindua mradi mkubwa wa maji wa Uwanja mpya wa Ndege wa Swaya mkoani Mbeya, huku akivirushia madongo kwa vyama vya upinzani kuwa vinafikiria kuanzisha ugomvi kila siku badala ya kuhamasisha maendeleo.

Rais Kikwete alisema atahakikisha anatekeleza ahadi zake zote alizoahidi wakati wa kampeni mwaka 2010 na kuhoji vyama vya upinzani vitawaeleza nini wananchi wakati wa uchaguzi mkuu mwaka 2015.


Akizungumza na wananchi wa Mbeya kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uzinduzi wa mradi mkubwa wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira uliopo Swaya, Rais Kikwete alisema kuna vyama vya siasa vya upinzani vinafikiria kuanzisha ugomvi.

Ingawa Rais Kikwete hakutaja jina la chama, lakini ni dhahiri kwamba alikuwa akikilenga chama kikuu cha upinzani nchini cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambacho ndani na nje ya Bunge kimejikuta kwenye mvutano na serikali kwenye masuala kadhaa yanayohusu maslahi ya taifa.

“Wengine wanatafuta ugomvi kila siku badala ya kuhamasisha maendeleo tuone mwaka 2015 watawaeleza nini wananchi, sisi chama chetu kinawahudumia wananchi wakati wengine wanawazuia wasiende kwenye miradi ya maendeleo, ikifanikiwa wao wanakuwa wa kwanza kuhitaji huduma wakati hawakushiriki kuhamasisha,” alisema Rais.

Akizungumzia mradi huo mkubwa wa maji uliogharimu sh bilioni 79.5, Rais Kikwete alisema umejengwa kwa ufadhili kutoka nchi za Jumuiya ya Ulaya iliyotoa sh bilioni 36.9, Ujerumani sh bilioni 13.5 na serikali sh bilioni 29.1 kupitia programmu yake ya maji.

Pia aliwaonya wananchi kuacha tabia ya kuharibu vyanzo vya maji na kuagiza kuwa wanapaswa kuvilinda na kuhifadhi miundombinu ya maji na kuvitaka vyombo vya dola kuwachukulia hatua wananchi watakaoshikwa wakiiba vifaa vya maji ambavyo vimenunuliwa kwa gharama kubwa.

Katika uzinduzi huo ulioshuhudiwa na Balozi wa Ujerumani hapa nchini, Klaus Brandes, alisema kuwa nchi yake imekuwa ikishirikiana na serikali tangu mwaka 1973 katika miradi mbalimbali ya maendeleo na itaendelea kufanya hivyo kutokana na ushirikiano mzuri uliopo kati ya nchi hizo mbili.

Naye Kamishina wa Maendeleo ya Jumuiya ya Ulaya, Andris Piebalgs, alisema kiasi hicho cha fedha kilichotolewa na jumuiya hiyo, kimesaidia kukamilisha mradi huo.

Uwanja wa Ndege wa Songwe
Kwa mara ya kwanza, Rais Kikwete jana alitua rasmi kwenye Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Songwe mkoani Mbeya akiwa kwenye ndege aina ya Forker 28 akiongoza msafara wa watu 31.

Kitendo cha Rais Kikwete kutua kwenye uwanja huo uliokamilika asilimia 95, kulimuongezea furaha zaidi katika ziara yake ya kuzindua mradi wa maji.
Baada ya kutua kwenye uwanja huo majira ya saa 5.15 jana, rubani wa ndege hiyo, Kapteni Dominick Boman, akiongozwa na Meneja wa Uwanja wa ndege wa Mbeya ilipotua, Valentine Kadeha, aliusifia kuwa una sifa zote za kurusha ndege kubwa zinazobeba abiria na kuhoji kwa nini haujaanza kutumika.

“Uwanja ni mzuri sana, sehemu ya kurukia ndege ni pana na uwanja ni mrefu hakika wananchi wana kila sababu ya kuufurahia, sijui kipi kinakwamisha kuanza kutumika kwa abiria labda vituo vya mafuta havijajengwa, suala la sehemu ya kushukia abiria si tatizo; marubani tunahitaji uwanja mzuri,” alisema Bomani.

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Viwanja vya ndege, Suleiman Suleiman, alisema uwanja huo utaanza kutumika rasmi Novemba Mosi.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...