Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Thursday, November 8, 2012

Uhuru Marathon: Mbio zitakazoiteka dunia


Na Mwandishi Wetu
FIKIRIA mbio zozote kubwa duniani kama vile London Marathon, Paris Marathon au yale mengine yenye kupendwa na wengi zaidi duniani ya Berlin Marathon.
Mashindano yote haya ni ya kutukuka kutokana na kushirikisha wanariadha wenye majina makubwa duniani, huku kukiwa na ushindani mkubwa zaidi miongoni mwa washiriki.
Sasa Tanzania inaweza ikapata kitu cha kujivunia zaidi kwa ujio wa mashindano ya mbio ndefu yaitwayo ‘Uhuru Marathon’ ambayo yanatarajiwa kuzinduliwa rasmi Desemba 5, mwaka huu jijini Dar es Salaam.
Upekee wa shindano hilo la Uhuru Marathon ni kutokana na aina ya washiriki wake, pamoja na kupewa tafu kubwa na waandaaji wa mashindano ya Berlin Marathon, ambao wanataka kuiona Tanzania inatangazwa zaidi.
Hivyo shindano la Uhuru Marathon, ndilo ambalo lina uwezo mkubwa wa kuwabeba Watanzania kwa kutangazika zaidi, hasa ukichukulia uzoefu mkubwa walionao waandaaji wa Berlin Marathon.
Hivi karibuni mjini Dodoma, Spika wa Bunge, Anna Makinda alifanya uzinduzi wa awali wa mbio hizo kabla ya uzinduzi wenyewe rasmi hapo Desemba 5. Mbio hizo ndefu zitakuwa zikiandaliwa na kuratibiwa na Kampuni ya Intellectuals Communication.
Akithibitisha hilo, Mratibu wa Uhuru Marathon, Innocent Melleck alisema lengo la mbio hizo ni kuwakumbusha Watanzania umuhimu wa kukumbuka, kuzingatia na kuuenzi urithi waliaochiwa na viongozi waliopigania uhuru wa nchi.
Alisema urithi huo ambao utakuwa ukikumbukwa kila mwaka kupitia mbio hizo ni upendo, mshikamano, umoja na amani iliyopo. Melleck aliisema mbio hizo zitakuwa zikifanyika kila mwaka na zitaanza rasmi hapo mwakani.
Melleck alisema pamoja na kwamba mbio hizo zimezinduliwa rasmi Bungeni pia wameandaa hafla ya uzinduzi mwingine jijini Dar es Salaam Desemba 5 katika hoteli ya Delemonte iliyopo Jengo la Benjamin Mkapa.
Mgeni rasmi katika uzinduzi huo anatarajiwa kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Dk. Fenella Mukangara.
Mratibu huyo alisema ana imani mbio hizo zitajizolea umaarufu mkubwa kutokana na jinsi zitakavyoweza kuteka hisia za watu mbalimbali wakiwemo wanamichezo.
Katika mbio hizo zitakazowashirikisha watu wa kada mbalimbali zitakuwepo pia mbio za kilomita 3, kilomita 5, kilomita 21 ambayo ni ‘half marathon’ pamoja na marathon yenyewe ambapo itakuwa na umbali wa kilomita 42.
Mratibu huyo alisema katika mbio za kilomita tatu itakuwa ni maalumu kwa ajili ya viongozi wa kada mbalimbali, wakiwemo pia wale wa dini na zile za kilomita 5 pia zitakuwa za kuchangia kwa ajili ya watu wa mahitaji ya kila aina.
“Hapa tunachotaka kufanya katika mbio za kilomita tatu ni kuwaomba kama vile viongozi maarufu wa dini mbalimbali pamoja na viongozi wetu ili kushiriki, kwa kudumisha amani na upendo.
“Pia tutahakikisha kama mbio za kilomita tano zinakuwa kwa ajili ya kuchangia watu wenye mahitaji mbalimbali na tayari tuna uhakika mkubwa wa wanariadha maarufu zaidi duniani watashiriki,” alisema.
Mratibu huyo alifafanua kuwa, wamejipanga mno katika hilo ili kuhakikisha wanafanya mambo makubwa zaidi na ambayo yataleta tija kwa taifa.
Wakati Uhuru Marathon ikitambulishwa bungeni, kiongozi aliyeonekana kufurahishwa zaidi na hilo na Spika Makinda, ambaye hakuishia kulimwagia sifa tu, bali alitaka hata viongozi wahakikishe wanalifanikisha.
“Ni wazo zuri hasa katika kipindi hiki ambacho tunapigania amani na mshikamano miongoni mwetu, kuenzi mashindano kama haya ili kutufanya tuwe wamoja zaidi,” alisema Spika Makinda.
Kwa nini Berlin Marathon?
Melleck alisema, wameanza mazungumzo na waandaaji wa mashindano ya Berlin Marathon, kwani hilo ni moja kati ya shindano kubwa zaidi duniani, likiwa linashirikisha wasanii mbalimbali walio maarufu zaidi.
“Tuko katika hatua ya mwisho ya kuingia mkataba wa ushirikiano na Berlin Marathon, naamini tutafika mbali zaidi katika kile ambacho tumedhamiria,” alisema Melleck.
Shindano la Berlin Marathon au maarufu zaidi kwa jina la BMW Berlin Marathon kutokana na kudhaminiwa na Kampuni ya BMW ni maarufu zaidi ndani ya Ujerumani na duniani kwa ujumla.
Shindano hilo lina umbali wa kilomita 42.195 na kushirikisha wanariadha wa kulipwa na wale wa ridhaa na lilianza kwa mara ya kwanza mwaka 1974 na linafanyika kila wiki ya mwisho ya mwezi Septemba ya kila mwaka.
Shindano hili kwa umaarufu wake mwaka 2008 lilishirikisha wanariadha wapatao 40,827 kutoka mataifa 107, huku waliomaliza mbio wakiwa 35,913 na lina zawadi kibao za kuvutia.
Uhuru Maratho watafaidikaje?
Melleck alisema ushirikiano wa Berlin Marathon una maana kubwa kwani itasaidia kuitangaza zaidi Tanzania na kuifanya dunia itambue umuhimu wa amani, upendo, umoja na mshikamano miongoni mwetu.
“Wanariadha wengi watashiriki katika mbio hizi wengi wakiwa maarufu zaidi duniani, pamoja na viongozi wa kada mbalimbali na hivyo kutimiza lengo tulilojiwekea.”
Mratibu huyo alisema, kuna kila haja kwa Watanzania kuyathamini mashanindano hayo, kwani yana lengo la kuwafanya wawe wamoja zaidi hasa katika kipindi hiki kigumu ambacho kuna majaribu ya kila aina.
“Waasisi wetu wa taifa na wale waliopigania uhuru walikuwa na malengo mengi na tunatakiwa kuyadumisha hayo, hilo ndilo Uhuru Marathon inalokwenda kupigania,” alisema.
Kwa Watanzania itakuwa faraja zaidi hasa ukichukulia jinsi taifa hili linavyoweza kufaidika kwa kuzalisha pia wanariadha wa aina mbalimba.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...