Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Thursday, September 12, 2013

Wanafunzi Darasa la Saba waanza mitihani ya kumaliza Elimu ya Msingi


https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEis4Qicfpp4xK5Mbq65CE9UaXyxXaPHmymyw2HcyzZpynC8wQZ9O6GusTdRfca1sibcJSZMp5Uju4q23T9Hx7OblB6IRDyK8ntqZUXybuong457GPg-Lytclj7KHAYGat0vhF2MYEg4Dvg/s640/MITIHANI+YA+DARASA+LA+SABA+MORO+2.jpg
Kazi itakuwa kama hivi, wengine wanajaza wengine wakitafakari kwa kina katika mitihani iliyoanza leo kwa wahitimu wa darasa la 7 nchini

JUMLA ya wanafunzi 868,030 wa Darasa la Saba nchini, leo na kesho wanatarajia kufanya mtihani wa kuhitimu elimu yao ya msingi katika  michepuo miwili, wa Kiswahili na Kiingereza.

Mitihani hiyo imeanza asubuhi ya leo katikma shule mbalimbali nchini, ambapo kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo, mtihani huo utakaojumlisha masomo matano, utafanyika kwa siku mbili kuanzia leo na kesho Alhamisi.

Kati ya idadi hiyo ya wanafunzi waliosajiliwa kufanya mtihani huo, wavulana ni 412, 105 sawa na asilimia 47, na wasichana 455, 925 sawa na asilimia 52.52. Jumla ya masomo matano yanatarajiwa kutahiniwa na wanafunzi hao ambayo ni pamoja na Kiswahili, Kiingereza, Sayansi, Hisabati na Maarifa ya Jamii.

Kwa mujibu wa Mulugo, wanafunzi 844, 810 wanatarajia kufanya mtihani huo kwa lugha ya Kiswahili, ambao kati yao wavulana ni 400, 335 na wasichana 444,575, huku 22, 535 watafanya kwa lugha ya Kiingereza, ambao wavulana ni 11, 430 ma wasichana 11, 105.

Mulugo alitaja kundi lingine la wanafunzi ambao wanakwenda kufanya mtihani kuwa ni pamoja na lile la wasioona ambao idadi yao ni 88, wavulana 56 na wasichana 32, huku wale wenye uoni hafifu na ambao wanahitaji maandishi makubwa ni 597.

Kati ya watahiniwa hao wenye uoni hafifu, wanaotarajia kufanya mtihani huo kwa lugha ya Kiswahili ni 546, wavulana 263 na wasichana 283, na wale watakaofanya kwa Kiingereza ni 51, wavulana 21 na wasichana 30.

Alisema maandalizi yamekamilika ikiwa ni pamoja na kusambazwa kwa fomu maalumu za OMR za kujibia mtihani na nyaraka zote muhimu huku akiwaagiza maafisa elimu wa mikoa na halmashauri kuhakikisha mazingira yanakuwa tulivu na kuzuia mianya yote ya udanganyifu wa mitihani.

Mulugo pia aliwataka wasimamizi  kusimamia kwa umakini na uadilifu wa hali ya juu.

Sambamba na hilo, aliwaasa wanafunzi wote kutojihusisha na vitendo vyovyote vya udanganyifu wa mtihani kwani watakaobainika kufanya hivyo watafutiwa matokeo yao yote ya mtihani.
MICHARAZO inawatakia kila la heri wanafunzi hao katika mitihani yao ili waweze kuifanya kwa amani na utulivu na ahatimaye wafaulu Inshallah.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...