Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Sunday, April 28, 2013

YANGA YAIVUTIA NGUVU SIMBA KWA KWENDA MAZOEZI YA GYM








PRESHA ya pambano la watani wa jadi imezidi kupanda, baada ya Yanga kujipa mazoezi ya nguvu kusaka pumzi na stamina kabla ya kuwavaa mahasimu wao, Simba, Mei 18 mwaka huu, huku viongozi na timu nzima wakidai kubakiza mechi hiyo kutimiza furaha yao.
Yanga, ambayo tayari imeshatangaza ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, imeona wazi kwamba hakuna sababu ya kubweteka na kusherehekea jambo hilo hadi hapo watakapomalizana na Simba katika mechi hiyo ya kusaka heshima kubwa.
Yanga imebainisha wazi kwamba furaha yao ya ubingwa wa ligi msimu huu haitakamilika kama watashindwa kuifunga Simba, hivyo jambo hilo limeifanya timu hiyo kuingia gym kupiga mazoezi ya nguvu kuhakikisha wanatunisha misuli, kutafuta stamina na pumzi ya kuhakikisha inawatuliza mahasimu wao kwa dakika zote tisini katika mechi hiyo itakayofanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Wababe hao wa mitaa ya Jangwani wamenyakua ubingwa huo kiulaini, baada ya Azam FC kuambulia sare ya bao 1-1 juzi katika mechi yake dhidi ya Coastal Union, matokeo ambayo yamefanya kusiwepo na timu yoyote inayoweza kufikia pointi za Yanga (56), huku timu hiyo inayonolewa na Mholanzi, Ernie Brandts, ikibakiza mechi mbili.
Lakini, sasa mabingwa hao wapya, Yanga wanadai furaha yao haijakamilika kwa sasa kwa sababu bado hawajawafunga Simba na hilo ndilo linalowafanya nyota wa kikosi hicho pamoja na benchi zima la ufundi kufanya mazoezi ya nguvu ili kuhakikisha wanakuwa fiti katika idara zote.
Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Clement Sanga, alisema wamepokea kwa mikono miwili ubingwa huo wa msimu huu, lakini bado wana kazi moja ya kuhakikisha mashabiki wa timu hiyo wanaendelea kupata furaha kwa kuwafunga watani wao wa jadi, Mei 18 mwaka huu.
Akisema hatua ya kupata ubingwa mapema ni ishara kwamba walikuwa wamejiandaa vyema, huku akiwapongeza wachezaji wake pamoja na benchi zima la ufundi kwa kufanya kazi kwa kujituma na kudai kwamba moto huo utaendelea hadi Mei 18 katika Uwanja wa Taifa.
“Tunaupokea ubingwa kwa furaha, lakini bado tuna kazi nyingine, moja ni kupata ushindi dhidi ya Coastal Union na pili ni kuifunga Simba katika mchezo wa mwisho, hizi ndizo changamoto kubwa zinazotukabili kwa sasa," alisema.
“Kwa hiyo tunawaomba mashabiki na wapenzi wa Yanga kuendelea kuiunga mkono timu hadi mwisho wa msimu kwa sababu tumedhamiria kuwapa raha.”
Katika hatua nyingine, Kocha mkuu wa kikosi hicho, Ernie Brandts ameeleza kuwa pamoja na kupata ubingwa huo wakiwa wamebakisha mechi mbili, lakini yeye bado hajamaliza ligi hadi atakapopata pointi sita zilizobakia kwenye michezo hiyo mwili.
“Ligi haijaisha, suala la kupata ubingwa ni jambo moja, lakini kumaliza kwa ushindi ni suala jingine muhimu zaidi, naamini kuwa hilo ni jambo ambalo limebakia kwangu na benchi langu la ufundi kuhakikisha kuwa tunapata pointi sita kutoka kwenye mechi zetu zilizobaki," alisema.
Kutokana na hilo, kocha huyo aliingiza timu yake katika mazoezi ya gym, katika kituo cha mazoezi kilichopo jengo la Quality Centre kujiandaa na mechi hizo mbili dhidi ya Coastal Union na Simba.
Kwa upande wa baadhi ya wachezaji waliozungumza jijini, wameeleza furaha yao kutokana na matokeo hayo, lakini wakisema kuwa wanayo kazi ya kulipa kisasi cha mabao 5-0 za msimu uliopita kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara.
Miongoni mwa wachezaji hao ni Mbuyu Twite, ambaye alidai ameupokea ubingwa huo kwa shangwe kubwa kwa sababu huu ni msimu wake wa kwanza na jambo zuri kumaliza ligi akiwa na medali ya ubingwa. Kiungo wa timu hiyo, Haruna Niyonzima, alisema jambo hilo linampa furaha kubwa na sasa anafikiria mpango wa kufanya mazungumzo ya kuweza kubaki kwenye kikosi hicho.
Yanga, ambayo kwa sasa imefikisha pointi 56 kwenye ligi baada ya kushuka dimbani mara 24, imebakiza mechi mbili dhidi ya Coastal Union itakayofanyika Mei Mosi na Simba itakayofanyika siku 18 baadaye, kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...