Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Tuesday, January 7, 2014

Msondo kumsindikiza Gurumo kuaga mashabiki jijini Tanga



Mzee Gurumo (kati) akiwa na waimbaji wa Msondo Ngoma, Tx Moshi Jr na Juma Katundu 'JK' enzi akiwajibika jukwaani
BENDI kongwe ya muziki wa dansi nchini Msondo Ngoma inatarajiwa kumsindikiza muimbaji wao za zamani na mwanamuziki mstaafu, Muhidini Gurumo katika onyesho maalum la kuwaaga mashabiki wake wa jijini Tanga.
Onyesho hilo ambalo ni muendelezo wa maonyesho maalum ya mkongwe huyo ya kuwaaga mashabiki wake nchini baada ya kuitumikiafani ya muziki kwa miaka zaidi ya 50, litafanyika Mkesha wa Siku ya Mapinduzi.
Msemaji wa Maseneta wa Msondo, Waziri Dewa aliiambia MICHARAZO kuwa, onyesho hilo la Tanga litafanyika Januari 11 kwenye ukumbi wa Tanga Hotel.
Dewa alisema katika onyesho hilo mashabiki watazawadiwa vitu mbalimbali kwa watakaowahi kuingia ukumbini na wale watakaoweza kuimba vyema nyimbo za muuimbaji huyo mstaafu maarufu kama 'Mjomba' na za bendi ya Msondo.
"Katika muendelezo wa kuwaaga mashabiki, Msondo itamsindikiza Gurumo jijini Tanga ambapo ataaga mashabiki siku ya Mkesha wa Siku ya Mapinduzi ambapo tutatoa zawadi kwa watakaoimba vyema nyimbo za Gurumo," alisema.
Dewa alisema miongoni mwa zawadi watakaopewa mashabiki hao ni pamoja na tisheti na CD za bendi hiyo hasa zenye nyimbo za zamani wa Msondo na zile zilizowahi kutungwa au kuimbwa na Gurumo mwenyewe.
Muhidini Mwalimu Gurumo alitangaza kustaafu muziki mwishoni mwa mwaka jana kutokana na matatizo ya afya na umri kumtupa mkono na aliagwa rasmi jijini Dar es Salaam Desemba 14 katika onyesho lililofanyika viwanja vya Sigara.
Mkongwe huyo ndiye aliyeiasisi bendi ya NUTA Jazz iliyokuja kufahamika kwa majina ya Juwata, OTTU na sasa Msondo, Mlimani Park iliyokuja kufahamika pia kama DDC Mlimani Park na Orchestra Safari Sound '(OSS) 'wana Ndekule'.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...