Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Friday, August 17, 2012

Lowasa atoa wito kwa viongozi wa Morogoro kushughulikia tatizo la kuchoma moto misitu


 Mh.Lowassa akiangalia madawati yaliyokabidhiwa kwa shule hiyo na Benki ya KCB hivi karibuni.
 Waziri Mkuu mstaafu Mh Edward Lowassa akikabidhiwa kibuyu na mama wa kimasai kata ya Mkundi wilaya ya Morogoro.Mh.Lowassa ni kiongozi wa jamii ya wamasai nchini.
  Waziri Mkuu mstaafu Mh Edward Lowassa akiwasalimia wanafunzi wa shule ya msingi ujirani katika eneo la wafungaji wa jamii ya wamasai kata ya mkundi wilaya ya Morogoro alikokwenda kukagua na kukabidhi harambe za wafugaji hao kwa ajili ya ujenzi wa shule yao hiyo.
****  **** ****
Waziri mkuu mstaafu mh Edward Lowassa ameuomba uongozi wa mkoa wa Morogoro kulishughulikia tatizo la uchomaji moto misitu.

Akizungumza mapema leo kwenye kijiji cha Kiegea mjini Morogoro,Mh.Lowassa  ametoa wito huo alipokuwa akikabidhi michango ya harambee ya wafugaji wa jamii ya Wamasai,kusaidia ujenzi wa shule ya msingi kijijini hapo.Mh Lowassa alialikwa kufanya kazi hiyo akiwa ni kiongozi wa jamii ya wamasai nchini.

Mh.Lowassa pia aligusia suala la baadhi ya wanchi kuwa na tabia ya kuchoma moto misitu hovyo hasa mkoa wa Morogoro,hali inayopelekea uharibifu mkubwa wa Mazingira,Lowassa amebainisha kuwa kila anapopita mkoani morogoro amekuwa akishuhudia misitu ikichomwa moto,hali iliyokuwa ikimhudhunisha sana.

''Nimekuwa nikishuhudia maeneo kadhaa ya misitu yakichomwa moto,kwa hivyo ndugu zanguni naomba tuachane na tabia hii pamoja na kuwa kilimo ni muhimu katika maisha yetu ya kila siku,lakini kwa njia hii tutaufanya mkoa huu wa Morogoro ugeuke jangwa'' alionya Lowassa na kuongeza kuwa iwapo mwanamuziki maarufu wa mkoa huo, Marehemu Mbaraka Mwinshehe angefufuka angesikitika sana.

''Mara nyingi nikikutana na hali hii,huwa naukumbuka wimbo wa Mbaraka Mwinshehe unaosema kuwa Morogoro maji yatiririka milimani, kama akifufuka atalia'' alisema Lowassa na kuuomba uongozi wa mkoa kushirikiana kwa pamoja kutafuta suluhisho la tatizo hilo ambalo limekuwa likikithiri siku hadi siku.''Mh DC wa Morogoro nawaombeni mtafute suluhisho la tatizo hili, tusipoangalia mkoa huu utakuwa jangwa''alisema.

Aidha Mh.Lowassa amesema kuwa suala la elimu ni muhimu zaidi kabla ya kilimo kwanza,akaongeza kuwa Elimu kabla baadaye kilimo kwanza.Mh Lowassa pia ametoa changamoto kwa wananchi wa kata mpya ya mkundi ya jamii hiyo ya wafugaji kuanza ujenzi wa shule ya sekondari ya kata.

''Ni aibu kata hii kutokuwa na shule ya sekondari wakati kila kata nchini ina shule ya sekondari ,ambako hivi sasa angalau kuna usawa kwa watoto kugusa elimu ya sekondari'' alisema na kuongeza kuwa atakuwa tayari kuja kwenye kata hiyo Januari mwakani kuongoza harambee ya kuchangisha fedha za ujenzi wa sekondari.Mh.Lowassa ndiye aliyeongoza operesheni ya ujenzi wa shule za kata kote nchini wakati alipokuwa waziri mkuu.

''Niko tayari kuja January kuongoza harambe ya kuchangisha fedha, ni aibu kwakweli sijafurahishwa na hali yenu hapa mnatakiwa nyinyi wenyewe msimame kidete kujiletea maendeleo, njooni Monduli mjifunze jinsi wafugaji wenzenu walivyoweza kutumia mifugo yao kujenga shule na nyumba za waalimu'' alisema Lowassa.

Mh.Lowassa amemtaka kila mfugaji kutoa ng'ombe au mbuzi mmoja kwa ajili ya kuchangia elimu kwenye kata yao na kumuomba mkuu wa wilaya kutumia sheria zilizopo kumkamata na kumtia ndani yeyote atakayekaidi wito huo.

Mh Lowassa alichangia mabati 500 kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa madarasa ya shule hiyo ya msingi ya Ujirani yenye wanafunzi 414 ,lakini yenye upungufu mkubwa wa Waalimu, wawili tu mmoja wa kuajiriwa na mwingine wa kujitolea.

Katika harambee ya wananchi wa eneo hilo walichanga ng'ombe watano kwa ajili ya kuendeleza shule hiyo, idadi ambayo mh Lowassa aliipinga,akidai kuwa ni Wanachi hao wana idadi kubwa ya mifugo hivyo walipaswa  kujitolea zaidi.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...