Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Thursday, June 27, 2013

TAMASHA LA WASANII MKURANGA LAAHIRISHWA KUMPOKEA OBAMA


TAMASHA la Mastaa Chipukizi lililokuwa lifanyike Jumamosi Juni 29 kijiji cha wasanii Mwanzega Mkuranga limeahirishwa ili kutoa nafasi kwa  wasanii na viongozi mbalimbali kushiriki kikamilifu katika maandalizi na mapokezi ya  Rais wa Marekani, Baraka Obama.
 
Mwenyekiti wa Mtandao wa Wasanii Tanzania (SHIWATA), Caaasim Taalib alisema jana kuwa wanachama wengi waliokuwa washiriki tamasha hilo watakuwa katika maandalizi ya ujio wa Rais Obama hivyo litafanyika mwezi Agosti baada ya sikukuu ya Idd el Fitri.
 
Taalib alisema anawaomba radhi wananchi wa Mkuranga, viongozi mbalimbali na wasanii washiriki wa tamasha hilo waliokuwa wamejiandaa kuonesha vipaji vyao katika tamasha hilo.
 
‘Tumeamua kutoa nafasi hii kwa wanachama wa SHIWATA ili washiriki kikamilifu kudumisha amani katika wakati huu ambao tunatembelewa na Rais Obama na wasanii washiriki kikamilifu, tunaomba tutoe taarifa katika vyombo vya dola mara tunapoona kuna unjifu wa amani’ alisema Taalib.
 
Mwenyekiti huyo alisema mgeni rasmi aliyekuwa ameandaliwa, Naibu Waziri wa Kilimo, Adam Malima amepelekewa ujumbe huo pamoja na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida na wabunge wa Dar es Salaam nao wamearifiwa kuhusu kusogezwa mbele tamasha hilo.
 
Alisema sambamba na tamasha hilo, SHIWATA ilikuwa ikabidhi nyumba kwa mchezaji wa zamani wa Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Jellah Mtagwa na wasanii wengine 14 ambao wamekamilisha michango ya ujenzi  wa nyumba zao katika kijiji chao cha Mwanzega Kimbili, Mkuranga.
 
Wengine watakaokabidhiwa nyumba zao ni msanii maarufu nchini, Lumole Matovola ‘Big’ wa Bongo movie ambaye ni wanachama wa SHIWATA wangine ni Mwandishi wa Habari, Josephine Moshi, Farida Ndimbo wa Jeshi la Magereza, Flora Kafwembe wa JKT Mgulani na Nyanza Kisadugwa wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).  
 
 Mpaka sasa SHIWATA imejenga nyumba 24 kwa ajili ya wasanii katika eneo la hekari 300 na wanajiandaa kulima shamba la hekari 500 walizonazo ili kujikwamua kimaisha.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...