Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Wednesday, May 21, 2014

JAPAN YAAHIDI KUENDELEA KUCHANGIA BAJETI YA TANZANIA


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akiwa katika mazungumzo na Katibu Mkuu Kiongozi wa Japan, Yoshihiro Suga, wakati alipofika ofisini kwake Jijini Tokyo Japan leo Mei 21, 2014, akiwa katika ziara ya kikazi.
****************************************************
 Mwandishi Maalum, Tokyo
Serikali ya Japan imeelezea nia yake ya kuendelea kuchangia bajeti ya Tanzania na kufafanua kuwa, inafanya hivyo kwa kutambua kuwa Tanzania ni mshirika mkubwa wa maendeleo na kwamba ni nchi yenye kutia matumaini katika kupiga hatua za kimaendeleo.
Akizungumza jana katika Ofisi yake jijini Tokyo, Katibu wa Baraza la Mawaziri wa Japan Mheshimiwa Yoshihide Suga alisema, serikali ya Japan inaifahamu Tanzania kama mshirika wa maana katika maendeleo na kwamba inafahamu mchango wa Tanzania katika kuendeleza ushirikiano wa nchi za Afrika Mashariki. Katibu Mkuu huyo pia aliongeza kuwa, Tanzania imemudu kudumisha amani kwa kipindi kirefu huku ikipiga hatua za kimaendeleo na kwamba watu wake wamebakia wamoja kwa miaka mingi licha ya kuwa na tofauti za kitamaduni, kijiografia na kidini.
Kauli hiyo ya Katibu wa Baraza la Mawaziri wa Japan, imetolewa kufuatia mkutano wake na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mohammed Gharib Bilal ambaye yupo jijini Tokyo kwa ziara ya kikazi. Katibu huyo alisema, “tunaifahamu Tanzania kama nchi muhimu inayodumisha amani. Nchi yenu imeweza kudumisha Muungano kwa miaka 50, Japan inawapongeza sana. Tunafahamu mnafanya kazi kubwa katika kuwaendeleza wananchi wenu na sisi kama ndugu na rafiki zenu tuko tayari kabisa kushirikiana nanyi.”
Katibu Mkuu Suga alieleza pia kuwa, Tanzania ni nchi iliyo thabiti katika ukanda wa Afrika Mashariki na inayo nguvu katika kuhakikisha ukanda huu unaendeleza utengamano hali ambayo inachangia kuwepo maingiliano ya wananchi wa ukanda wa Afrika Mashariki sambamba na kutanua fursa kwa wawekezaji kutoka nje ya Afrika.
“Mko thabiti katika mambo mengi na hasa kuweza kumudu kuwa na amani na utulivu, mnategemewa sana na nchi za Afrika Mashariki na kwa hali hii sisi tupo tayari kuendelea kutenga fedha katika bajeti yetu kwa ajili ya kusaidia miradi mbalimbali ya Tanzania katika ushirikiano wa serikali na sekta binafsi (PPP),” alisema.
Kwa upande wake Mheshimiwa Makamu wa Rais Dkt. Bilal alimueleza Katibu Mkuu Suga kuwa, Tanzania inapokea kwa heshima kubwa mchango wa Japan kwa kutambua hali yake ya utulivu na kwamba anatumia ziara yake Japan kuhamasisha wawekezaji kuja kuwekeza Tanzania.
“Tuna kazi kubwa mbele yetu katika kuwaendeleza Watanzania. Hatuwezi kufanya kazi hiyo peke yetu, hivyo basi nitumie nafasi hii kukuomba Mheshimiwa Katibu Mkuu kutusaidia kuhamasisha wawekezaji kutoka Japan ili waje kushirikiana nasi katika kuiendeleza Tanzania. Urafiki kati yenu na sisi ni wa siku nyingi na tungetegemea sasa tuubadili na utazame fursa za kuchangiana kiuchumi na hasa katika kuwekeza kwa kubadilishana teknolojia pamoja na mtaji,” Makamu wa Rais alisema.
Mheshimiwa Makamu wa Rais yuko nchini Japan kwa ziara ya kikazi na tayari amefanikiw akukutana na wakuu wa makampuni mbalimbali makubwa duniani yenye makao yake makuu nchini Japan na kisha kutumia nafasi hiyo kuelezea fursa za uwekezaji nchini Tanzanja sambamba na kubainisha umuhimu wa sekta binafsi kushiriki katika kusaidia maendeleo ya nchi zinazoendelea zilizopo Afrika, Tanzania ikiwa ni kipaumbele.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...