Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Monday, May 12, 2014

BALOZI IDDI ATEMBELEA KUJIONEA NYUMBA YA SALIM AHMED SALIM ILIYOBOMOKA MJINI ZANZIBAR, AKUTANA NA WAWEKEZAJI WA INDIA


 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akijumuika pamoja na baadhi ya wananchi kuangalia athari iliyotokea na  nyumba ya Bwana Salim Ahmed Salim baada ya ukuta na dari yake kuanguka  saa sita usiku juzi mkabala na Skuli ya Sekondari ya Tumekuja Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar.
 Sehemu ya mbele ya Nyumba ya Bwana Salim Ahmed Salim iliyoporomoka  Mtaa wa Vuga mkabala na Skuli ya Sekondari ya Tumekuja.
Hata hivyo hakuna mtu aliyejeruhiwa kutokana na athari hiyo.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akizungumza na Meneja wa Kampuni ya Kimataifa ya uwekezaji vitega uchumi  wa Kampuni ya Lucky Exports kutoka Nchini India Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
 Balozi Seif akisalimiana na Menaja wa Kampuni ya Lucky Exports ya India inayotaka kuwekeza katika sekta za Afya na Viwanda vidogo vidogo vya mazao ya Baharini.
Balozi Seif akisalimiana na Mwakilishi wa Kampuni ya Lucky Exports Tawi la Tanzania Bwana Kim Mghaya. Kati kati yao ni Meneja wa Kampuni hiyo yenye makao makuu yake Nchini India Bwana Ravi  Rai.
*********************************
Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar, Jeshi la Polisi pamoja na Mamlaka ya Usafiri zimekumbushwa kuendelea kuzuia uingiaji wa  gari kubwa zenye uzito wa zaidi ya Tani Mbili katika eneo la Mji Mkongwe ili kunusuru majengo yaliyono ndani ya mamlaka hiyo.
Kumbusho hilo limetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipofanya ziara fupi  kukagua athari ya nyumba  iliyoporomoka ukuta na Dari yake juzi usiku iliyopo Mkabala na Skuli ya Sekondari ya Tumekuja  Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar.
Balozi Seif alisema ukaidi wa baadhi ya madereva  wa gari kubwa kupitisha Gari gari zao katika eneo hilo umesababisha uchafuzi wa mandhari na haiba ya Mji mkongwe wa Zanzibar ambao hivi  sasa uko katika urithi wa Kimataifa.
“ Jeshi la Polisi wakati huu litahitajika kuwa na kazi ya ziada katika kuhakikisha agizo lililotolewa na Mamlaka ya Mji Mkongwe wa Zanzibar  linatekelezwa ipasavyo “. Alisisitiza Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akimpa pole Mmiliki wa Nyumba hiyo Bwana  Salim Ahmed Salim  kwa hasara  aliyoipata alimtaka kuwasiliana na Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar  katika juhudi zaujenzi wa nyumba hiyo utakaozingatia  mpango  halisi wa uhifadhi wa Mji huo.
Akitoa ufafanuzi wa athari nyingi zilizojitokeza ndani ya nyumba za Mji Mkongwe, Mkuu wa Kitengo cha Ushirikiano na Utafiti cha Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar Bibi Madina Haji Khamis alisema ujenzi usiozingatia utaalamu wa Mamlaka  husika pamoja na upitishwaji wa gari kubwa ndio sababu kubwa za msingi za athari hizo.
Bibi Madina alifahamisha kwamba baadhi ya  wamiliki wa nyumba hizo walikuwa wakipandishia kuta  wakati wa ujenzi au matengenezo zaidi ya uwezo wa msingi wa nyumba hizo hali  inayoleta athari ya mipasuko ya nyumba hizo sambamba na mitetemeko ya gari kubwa zinazopitishwa pembezoni mwa nyumba hizo.                           
Mapema Mmiliki wa Nyumba hiyo Bwana Salim Ahmed Salim alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Balozi Seif kwamba dalili za kuanguka kwa jengo hilo zilijionyesha mapema kutokana na kuvimba na baadaye kupasukwa kwa eneo la mbele la ukuta wa nyumba hiyo.
Bwana Salim alifahamisha kwamba kutokana na hali hiyo alilazimika kuuarifu Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar uliolazimia baadaye kwa kushirikiana na jeshi la Polisi kuchukuwa hatua za kuifunga bara bara hiyo.
“ Nilijaribu kuufuata Uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe uniruhusu kuifanyia matengenezo makubwa nyumba yangu  ili baadaye niitumie kwa makazi na familia nyangu lakini bado sijapata jibu na huku inaporomoka “. Alieleza Bwana Salim Ahmed Salim.
 Nyumba hiyo ya ghorofa moja mpaka inaporomoka ukuta na dari yake majira ya saa sita juzi usiku lakini hamna watu waliokuwa wakiishi ndani yake.

Mamlaka ya Mji Mkongwe wa Zanzibar kwa kushirikiana na Taasisi nyengine zimelazimika  kuzuia  Gari zote zinazotumia  Bara bara hiyo kutoka Vuga kuingia Shangani au kupitia Serena  ili kujaribu kuepuka hatari katika kipindi hichi cha Mvua za Masika.
 Kwa mujibu wa hali halisi ilivyo hivi sasa gari zote zinazokusudia kuingia ndani ya eneo la Mamlaka ya Mji Mkongwe zinalazimika kutumia Bara bara itokayo Malindi na zisizidi uzito wa zaidi ya Tani mbili.
Mamlaka ya Hifadhi ya Mji Mkongwe wa Zanzibar kwa miaka kadhaa sasa imo ndani ya Ramani ya Dunia ya urithi wa hifadhi ya Kimataifa chini ya usimamizi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu,Sayansi na Utamaduni  { UNESCO }.
Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alikutana kwa mazungumzo na ujumbe wa Kampuni ya uwekezaji vitega uchumi vya sekta za Afya, Kilimo, Umeme, viwanda vidogo vya mazao ya Baharini ya Lucky Exports kutoka Nchini India.
Kampuni hiyo ambayo imefungua Matawi yake katika mataifa mbali mbali Barani Afrika tayari imeshapata usajili wa kufungua Tawi lake Nchini Tanzania.
Katika mazungumzo yao yaliyofanyika Ofisini kwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar  Meneja wa Kampuni hiyo Bwana Ravi Rai  alisema Taasisi yake imelenga kutoa huduma za afya pamoja na viwanda vidogo vidogo vya mazao ya Baharini.
Bwana Ravi Rai alisema wakati Uongozi wa Taasisi yake ukisubiri kuanza na hatimae kukamilisha taratibu zote za uwekezaji uwekaji wa miradi hiyo umekusudia kusaidia kutoa ajira kubwa kwa wazalendo pamoja na kuongeza mapato ya Taifa.
Alifahamisha kwamba utafiti  wa wataalamu wa Taasisi hiyo utafanywa ili kuangalia miradi ambayo kampuni hiyo inaweza kuiwekeza hapa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.
“ Tunafarajika kuona kwamba miradi yoyote tutakayoamuwa kuitekeleza  kwenye uwekezaji wa mataifa mbali mbali duniani na hasa tukilenga zaidi Bara la Afrika inafadhiliwa na Serikali ya India “. Alisema Meneja huyo wa Lucky Exports.
Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema miradi iliyofikiriwa kuanzishwa na Uongozi wa Kampuni hiyo hapa Zanzibar  ya Sekta ya Afya na Viwanda Vidogo vidogo vya mazao ya Baharini  itasaidia kustawisha maisha naustawi wa Jamii Nchini.
Balozi Seif aliuagiza  Uongozi wa Kampuni hiyo ya Lucky Exports kutoka Nchini India kurahisisha maombi yao ya uwekezaji ili taasisi zinazohusika na uwekezaji ziweze kuyapitia na kutoa maamuzi yanayostahiki kwa wakati muwafaka.
Kampuni ya Uwekezaji ya Lucky Exports ya Nchini India ambayo tayari imeshafungua matawi yake katika Mataifa ya Ethiopia, Guinea Bisau,  Malawi na Tanzania inajihusisha zaidi na uwekezaji wa miradi ya Afya, Kilimo, Viwanda vya mazao ya Baharini, Umeme pamoja na huduma za Reli.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...