Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Saturday, July 27, 2013

WAKAZI WA MKOA WA LINDI WATAKIWA KUHAKIKISHA VIJANA WAO WANAKUWA NA UADILIFU


Na Anna Nkinda – Maelezo, Lindi
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete amewataka  wakazi wa mkoa wa Lindi kuhakikisha kuwa vijana wao wanaishi maisha ya uadilifu, wanamcha  Mwenyezi Mungu na kusoma elimu ya Dunia ili wasipotee  katika Ulimwengu wa utandawazi.
Mama Kikwete ametoa wito huo  jana wakati wa futari iliyowajumuisha  viongozi mbalimbali wa Serikali  na vyama vya siasa mkoani Lindi.
Alisema kuwa ni jambo jema kwa binadamu kuishi maisha ya kumpendeza Mwenyezi Mungu kwani hatuna mtu anayejua siku yake ya kufa hivo basi ni muhimu kujiandaa  mapema kwa kutenda matendo mema  ili ukifika huko uwe na mazingira mazuri ya baadaye na  hakuna cha kusema kuwa  mimi ni mdogo bado kwani kwa Mungu hakuna cha mdogo wala mkubwa.

“Kufunga kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani ni lazima kwani ni moja ya ibada katika kutengeneza afya ya mwili wako na kuwa karibu na Mwenyezi Mungu na ndiyo maana  hata watoto wadogo wanatakiwa kujifunza kufunga.

Lakini siku hizi kufunga imekuwa ni  mtihani kwa baadhi ya watu kuna  wengine wanasingizia ugonjwa ili wasifunge jambo ambalo si sawa kwani kuna baadhi ya watu wanaugua ugonjwa wa kisukari na wanafunga lakini hawapati matatizo kwakuwa ukidhamiria utafunga tu bila tatizo hata kama ni  mgonjwa na Mwenyezi Mungu atakupa uzima”, alisema Mama Kikwete.

Aidha Mama Kikwete pia aliwataka viongozi hao wa Serikali na vyama vya Siasa kutunza amani iliyopo kwakuwa  amani ni tuzo ya  taifa na nchi bila ya kuwa na amani haikali  na  hakuna jambo lolote linaloweza kufanyika kwani hata wanyama watapata tabu na kukosa mahali pa kuishi.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Lindi Ludovick Mwananzila alimshukuru Mama Kikwete kwa futari aliyoiandaa kwa ajili yao na kusema kuwa dini zote zinahimiza umuhimu wa kusali na kutubu hivyo basi ni jukumu la kila mtu kufanya hivyo.
Mkuu wa mkoa huyo alisema kuwa kila mtu anatakiwa kumcha Mungu na kumtukuza bila kusahau kuwasaidia watu waliopo katika dhiki ambao wanatakiwa kusaidiwa kwa kufanya hivyo watapata  thawabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Naye Shekhe na Kadhi mkuu wa mkoa wa Lindi Mohamed Mushangani alisema kuwa utaratibu wa watu wa aina mbalimbali kukutana  na kufanya jambo kwa pamoja kunawafanya wapendane zaidi kwani mtu akikupenda nawe utampenda, hivyo basi wawe na mapenzi na kupendana ili wapate raha katika maisha.
Alisema kuwa katika kumi la pili la kufunga ni la msamaha kama alivyosema Mtume Swalallahu Alayhi Wassalam (S.A.W) hivyo basi kwa wale wanaofunga wanatakiwa kujikita zaidi katika kufanya mambo mazuri kwa watu ikiwa ni pamoja na kulisha wengine kwani  ukimpa kula na kunywa mwenzako Mwenyezi Mungu anakulipa zaidi.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...