Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Sunday, July 21, 2013

Maskini! Papii Kocha alilia tena Rais Kikwete


MUIMBAJI Nyota wa zamani wa bendi ya FM Academia, Papii Kocha amemuandikia ombi jingine maalum Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete kumuomba MSAMAHA wa kufutiwa adhabu yake ya kifungo cha maisha jela alichopewa yeye na wanafamilia yake kwa kesi ya kubaka.
Ujumbe huo unaelezwa ni wa mara nyingine tena kwa msanii huyo aliyepo gerezani na baba yake, japo hakujawa na hakika kama barua hizo zinamfikia Mheshimiwa na kuzisoma au la. Ebu isome mwenyewe barua hiyo ya 'Mwana Mfalme' Papii Kocha kwenda kwa Rais Jakaya Kikwete...inaumiza!
MF/NA: 836'04 Johnson Nguza

(Papii Kocha) Gereza Kuu Ukonga

S.L.P 9091

Dar es Salaam
Mh. Rais Jamuhuri ya Muungano Tanzania

YAH: MAOMBI YA KUPEWA MSAADA (MSAMAHA) WA KUFUTIWA ADHABU YA KIFUNGO NILIYOPEWA NA MAHAKAMA YA HAKIMU MKAZI KISUTU.

Husika na somo hilo hapo juu. Mimi ni mfungwa katika gereza kuu Ukonga. Kwa heshma na taadhima na kwa kutambua utu na huruma yako ya kiMUNGU ulionayo dhidi ya binadamu wenzako pamoja na mamlaka uliokabidhiwa na Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Naanguka na kushika miguu yako mitukufu muheshimiwa rais....Nakuomba msaada (msamaha) kwako muheshimiwa rais, kwa njia hii ya maandishi kusudi niweze kuondolewa adhabu ya kifungo cha maisha gerezani, niliyohukumiwa na mahakama tajwa hapo juu. Mh.Rais mimi nimefungwa nikiwa bado kijana mwenye umri mdogo, na ukweli kutoka moyoni sikufanya kosa hilo.

Si mimi, baba yangu Nguza wala ndugu yangu yeyote aliyefanya kitendo kile. Lakini wenye mamlaka wakatuona tuna hatia na kuamua kuteketeza kizazi chetu gerezani.

Natamani kiama ifike ili mwenyezi Mungu aweke wazi ukweli wote uliojificha nyuma ya pazia. Mpaka sasa natambua wazi hatima pamoja na dhamana ya maisha yangu ipo katika mikono yako mitukufu Mh. Rais Naomba huruma yako muheshimiwa Rais maana mimi ni mtoto wako ninaehitaji huruma yako wewe mzazi. Lakini pia sisi ni binadamu wenye nafsi na miili kama wengine. Waliotumia mamlaka yao kutuweka gerezani nao ni binadamu pia, wenye miili na nafsi.

Ipo siku nafsi zetu zitapaswa kutoa hesabu ya tuliyoyafanya hapa duniani. wakati huo miili yetu tunayoitumia kunyanyasa wanyonge itakuwa imeoza mavumbini.

Natumaini kauli yako ya mwisho ndio itakayoleta pumzi ya uhai nafsini mwangu. Nakutakia kazi njema, afya njema na maisha marefu. Mungu akubariki. Wako mtiifu

Mfungwa NO:836'04 JOHNSON NGUZA (PAPII KOCHA)

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...