Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Wednesday, June 4, 2014

EFM 93.7 'YA MKUDE SIMBA' YAZINDULIWA KWA BONGE LA SHOO, DULLY ACHAFUA HALI YA HEWA MASHABIKI WATAWANYWA KWA MABOMU


 Jukwaa la shoo hiyo, lilivyokuwa.
Msanii, Dogo Kinagana, akionyesha umahiri wake wa kucheza na Sayansi kwa kunywa maji chupa nzima na kisha kuanza kuyatoa kwa kufinya sikio lake, wakati wa shoo baab kubwa ya uzinduzi wa Kituo cha Redio mpya ya EFM, iliyofanyika kwenye Viwanja vya Mwembe Yanga Temeke jijini Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki iliyopita.
**************************************************

Na Mwandishi Wetu, Dar

Katika shoo hiyo pamoja na kubamba na kuhudhuriwa na wananchi kibao na mashabiki wa burudani, lakini iliingia dorasi baada ya kwenda vizuri hadi hatua za mwisho kwa kupanda wasanii wote na hasa wale wa miondoko ya Mnanda na baadaye wale wa Bongo Flava.

Ommy Dimpoz na Dully Sykes, walikuwa ni miongoni mwa wasanii wa mwisho kupanda jukwaa hilo, ambapo alipopanda Ommy Dimpozi, mashabiki walianza kuonyesha dalili za kutomkubali na kuanza dalili za kutaka kumzomea, na ndipo Dimpoz, aliposhitukia issue na kwenda na alama za nyakati kwa kusimamisha muziki na kuzungumza na mashabiki hao.

''Oya Mashabiki wangu, kwa upande wangu naamini nisingeweza kuwa hapa ama kufikia hapa nilipo na kujulikana kitaifa na kimataifa bila ninyi, kwa kutambua mchango wenu kwangu, natamani hata kidogo nilichonacho tugawane'', alisema huku akichomoa mkwanja mfukoni

Baada ya maneno hayo alianza kwa kurusha Kofia yake kwa mashabiki, ambao walianza kuigombea kama mpira wa kona, akaona bado haitoshi na kurusha miwani yake na kisha akawachangaya zaidi kwa kurusha Sh. 30, 000 na hapo ndipo balaa lilipoanzia ambapo mashabiki walikanyagana kwa kugombea pesa hizo.


Dimpozi, alipoona zogo lile likiendelea huku mashabiki hao wakigombea kitita hicho, aliamua kuwamaliza kabisa kwa kuchomoa Sh. 200, 000 na kuzirusha hewani ambapo sasa ilikuwa ni patashika nguo kuchanika, na hapo sasa aliyefanikiwa kupata alipata huku wengine wakiambulia vipande tu vya noti hizo.

Na wakati wakigombea pesa hizo sasa Dimpoz alianza kuwarusha kwa nyimbo zake zinazobamba nao bila hiyana walisahau yote na kuanza kucheza huku wakimshangilia kwa nguvu zote hadi alipomaliza na kushuka jukwaani.

Balaa kubwa liliibuka pale alipopanda msanii wa mwisho kumalizia shoo hiyo, ambaye alikuwa ni Dully Sykes, ambaye baada ya kusalimia tu, Jamaa walianza kwa kumpiga na malapa, kisha wakafuata na kurusha mchanga, na kisha mawe na hatimaye sasa wakaanza kurusha chupa, ambayo moja wapo ilimjeruhi mmoja wa askari aliyekuwa eneo hilo la jukwaani akilinda amani.

Hapo ndipo Askari wa kutuliza ghasia walipoamua kuingilia kati kwa kuwatawanya mashabiki hao kwa kufyatua risasi hewani na mabomu ya machozi, ambayo hata hivyo bado watoto hao wa TMK, walionekana kutoyaogopa na kuendelea na kufanya fujo huku watu wakikimbia hovyo kutoka eneo hilo kujisalimisha na shoo ikawa imeishia hapo.

Juni 15, Shoo hiyo ya utambulisho wa ujio mpya wa EFM inatarajia kuendelea katika Wilaya ya Kinondoni ambapo inatarajia kufanyika katika Viwanja vya Biafra.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...