Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Tuesday, November 19, 2013

MKUU WA MKOA WA RUKWA AMTEMBELEA MAMA MARIANNE MJERUMANI ALIYEHAMIA TANZANIA NA KUJITOLEA KULEA WATOTO YATIMA 12


Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Injinia Stella Manyanya akiteta jambo na Mama Marianne Lwanetzki  raia wa Ujerumani alipomtembelea nyumbani kwake jana kujionea maisha ya mama huyo ambae kwa sasa anaishi Mkoani Rukwa katika nyumba yake inayoitwa 'Kinder House" na watoto yatima 12 ambao aliamua kuwachukua kutoka katika mazingira magumu na kuishi nao kama watoto wake huku akiwapatia huduma mbalimbali za chakula, malazi, elimu na tiba. Watoto hao yatima wapo wanaume sita na wanawake ni sita.

Katika historia yake fupi Mama huyo alifika Mkoani Rukwa kwa shughuli za kitalii na ndipo alipomuona mtoto mmoja katika moja ya kituo cha kulelea mayatima akiwa na hali mbaya ya kiafya huku akiwa mgojwa sana, Aliamua kumchukua mtoto huyo na kuishi nae hadi akapona ndipo aliposhawishika na kuamua kuhamia Tanzania na kuchukua watoto wengine yatima hadi kufikia 12 ambao kwasasa amesema wanatosha kulingana na uwezo alionao.

 Aliongeza kuwa katika kuwalea watoto hao anatumia uwezo wake yeye binafsi pamoja na misaada  mbalimbali kutoa kwa ndugu, jamaa na marafiki wa nchini kwake Ujerumani.
Mtoto Kastory Mabruki ambaye ametajwa kuwa na sifa mbalimbali ikiwemo Uongozaji wa kwaya kama inavyoonekana pichani na hata uongozaji wa midahalo"debate" mbalimbali shuleni kwao zikiwemo za wanafunzi wa madarasa ya juu zaidi ya lile analosoma na kuzimudu vizuri. Katika watoto hao 12 kila mmoja anaonekana kuwa na kipaji cha aina yake ambapo Mama yao Mlezi anajitahidi kuviendeleza na kuvipa nafasi.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Injinia Stella Manyanya akiongea kumpongeza Mama Marianne kwa juhudi alizozichukua ambapo ameguswa sana na mpango huo wa mtu binafsi kulea watoto kama familia moja tofauti na sehemu nyingine nyingi ambazo taasisi ndizo zinazojishughulisha na vituo vya kulelea mayatima. Mkuu huyo wa Mkoa amewaasa watanzania wenye uwezo kuiga mfano huo kusaidia jamii kuondokana na kero za watoto wa mitaani.
Picha Ndani: Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Injinia Stella Manyanya (katikati mbele waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mama Marianne Lwanetzki (wapili kushoto mbele waliokaa) raia wa Ujerumani na watoto yatima 12 alioamua kuwachukua na kuwalea kama watoto wake wakitokea katika mazingira magumu na ambao anaishi nao katika nyumba yake anayoiita "Kinder House" iliyopo katika Manispaa ya Sumbawanga Mkoani Rukwa. Mama huyo anawapatia watoto hao mahitaji yao yote ikiwemo chakula, malazi na elimu. Kulia ni Katibu wa Mhe. Manyanya Frank Mateni. 
 Picha Nje: Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Injinia Stella Manyanya (watatu kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mama Marianne Lwanetzki (watatu kulia) raia wa Ujerumani na watoto yatima 12 alioamua kuwachukua na kuwalea kama watoto wake wakitokea katika mazingira magumu na ambao anaishi nao katika nyumba yake anayoiita "Kinder House" iliyopo katika Manispaa ya Sumbawanga Mkoani Rukwa. Mama huyo anawapatia watoto hao mahitaji yao yote ikiwemo chakula, malazi na elimu. Wapili kulia ni Hamza Temba - Afisa Habari Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa.
Handshaking.
Nyumba hii inajulikana kama "KINDER HOUSE" ambapo kwa mujibu wa Mama mwenye nyumba hii Marianne Lwanetzki ambae ni raia wa Ujerumani alisema neno "kinder" kijerumani lina maana ya watoto. Mama Marianne amesema nyumba hiyo ambayo ni kubwa ikiwa na eneo la kutosha ameshaiandikia kisheria na kwamba ni urithi kwa watoto hao 12 anaowalea hata kama hatokuwepo tena duniani basi hapo ndipo nyumbani kwao.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa akiagana na familia ya Mama Marianne Lwanetzki yenye watoto yatima 12 pamoja na wafanyakazi wake wanaomsaidia kwenye shughuli za malezi. (Na Hamza Temba - Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa @Rukwareview.blogspot.com)

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...