Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Friday, July 9, 2010

OLIMPIKI AFRIKA KUANZA JUMATATU


bendera ya Tanzania ikipepea wakati wa michuano hiyo iliyofanyika miaka iliyopita
WATANZANIA wameombwa kuwaunga mkono na kuwaombea dua wanamichezo wanne ambao wanaondoka nchini kesho kwenda kuiwakilisha nchi katika mashindano ya kwanza kwa vijana ya Olimpiki Afrika (ANOKA) yanayoanza jumatatu Rabat nchini Morocco.



Akizungumza Dar es Salaam leo wakati wa kuwakabidhi wanamichezo hao bendera ya Taifa , ambao watashiriki katika mchezo wa riadha na kuogelea, Mkurugenzi wa Michezo Zanzibar Gulam Rashid alisema, wanamichezo hao wanatakiwa kuungwa mkono na kila mtanzania kutokana na kwamba wanashiriki kwa mara ya kwanza mashindano makubwa kama hayo huku wakiwa ni vijana wadogo.



"Tunatakiwa kuwaunga mkono na kuwaombea dua ili waweze kufanya vizuri na kuiwakilisha vyema nchi, hivyo kila mtanzania anatakiwa kuwaunga mkono kwa kuwapa sapoti hata watakapokuwa wameshindwa kwani hayo ni mashindano na nchi nyingi zinashiriki na si kuwaandika vibaya katika vyombo vya habari,"alisema Rashid.



Wanamichezo hao kwa upande wa riadha ni Marwa Mwita atakayekimbia meta 1,000 na 3,000 ambao wataambatana na mwalimu wao Meta Petrol ambapo wanariadha hao waliweka kambi mjini Arusha.



Kwa upande wa kuogelea ni Adam David atakayeogelea umbali wa meta 50 pamoja na Mariam Foum ambaye pia ataogelea umbali huo huo kwa stail ya Freestyle.



Naye Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) Filbert Bayi alisema Kwa mara ya kwanza Kamati ya Olimpiki ya Kimataifa (IOC) ilizindua kwa mara ya kwanza michezo ya Olimpiki kwa vijana chini ya miaka 17 mwanzoni mwa mwaka 2008 na kupendekezwa Singapore kuwa mwenyeji wa michezo hiyo.


"Kamati za Olimpiki za nchi wanachama zilialikwa kushiriki aidha kwa kufikia viwango vilivyotolewa na vyama vya kimataifa au kuomba nafasi za upendeleo ,"



"Kwa kuzingatia vyama vyetu kutokuwa na idadi kubwa ya vijana wenye umri huo ambao wangeweza kufikia viwango, TOC, iliomba nafasi ya upendeleo kwa vyama vya riadha, kuogelea, mpira wa meza na ngumi lakini IOC ilitupa nafasi kwa michezo miwili rianda na kuogelea,"alisema Bayi.



Wanamichezo hao wanatarajia kuondoka leo na ndege ya shirika la Qatar ambapo mkuu wa msafara atakuwa ni Peter Mokani ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Olimpiki Tanzania TOC.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...